Skip to main content

Uchaguzi DRC 2018: Kwa nini huenda Rais Joseph Kabila akawania urais tena 2023

  Bw Kabila Kinshasa 9 Desemba, 2018
 Bw Kabila anasema bado safari ni ndefu

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Joseph Kabila amesema ataendelea kushiriki katika siasa nchini humo hata baada ya kuondoka madarakani baada ya uchaguzi utakaofanyika wiki mbili zijazo.
Aidha, hajafutilia mbali uwezekano wake wa kuwania tena urais uchaguzi mkuu mwingine utakapoandaliwa mwaka 2023.
Bw Kabila alitarajiwa kuondoka madarakani miaka miwili iliyopita baada ya kuongoza kwa mihula miwili kwa mujibu wa katiba.
Hata hivyo, uchaguzi mkuu nchini humo uliahirishwa mara kadha, serikali ikisema maandalizi yake hayakuwa yamekamilika vyema.
Upinzani ulitazama hilo kama njama ya Bw Kabila kutaka kuendelea kuongoza.

Mwezi Agosti, Bw Kabila alimtangaza mshirika wake wa karibu Emmanuel Ramazani Shadary ambaye ni waziri wa zamani wa mambo ya ndani kuwa mgombea wa muungano wa kisiasa unaotawala kwa sasa.
Bw Shadary amewekewa vikwazo na Umoja wa Ulaya kutokana na tuhuma za ukiukaji wa haki za kibinadamu.
Katibu wa chama cha upinzani cha Movement for the Liberation of Congo (MLC), Eve Bazaiba, ameambia BBC kwamba Bw Shadary atadhibitiwa na Bw Kabila na kwamba kimsingi itakuwa ndiye anayeongoza nchi.
"Anataka tu kusalia madarakani. Hata kama alimchangua Shadary, Shadary ni mtu tu wa kuonekana, ndiye atakayemuongoza Shadary kwa kila jambo. Kiuhalisia, atakuwa bado ndiye rais."
Bi Bazaida amesema serikali imekuwa ikiwazuia wanasiasa wa chama cha MLC kufanya kampeni.
Emmanuel Ramazani Shadary
Kwa muda mrefu, ilikuwa bado haijabainika iwapo Rais Kabila, angewania tena hadi alipoamua kumtangaza Shadary kuwa mgombea wa muungano wake wa kisiasa.

Kwenye mahojiano na shirika la habari la Reuters, Rais Kabila amesema: "Mbona tusisubiri hadi mwaka 2023 … ndipo tuwe na uwazi kuhusu mambo haya," alisema.
"Maishani sawa na ilivyo katika siasa, hauwezi kufutilia mbali jambo kabisa."
Kumekuwa na wasiwasi kutoka kwa upinzani na jamii ya kimataifa kuhusu iwapo uchaguzi wa DRC utakuwa huru na wa haki.
Lakini Bw Kabila amesema wasiwasi huo haufai kuwepo.
Martin Fayulu Novemba 11, 2018 Geneva
 Martin Fayulu awali alitangazwa kuwa mgombea wa muungano wa upinzani


"Tunakusudia kadiri ya uwezo wetu kuhakikisha uchaguzi huu hauna kasoro hata moja. Waangalizi wanaofikiria kwamba uchaguzi huu hautakuwa huru na wa haki, bado sijawaona wakija hapa na kusema ni kitu gani tumekikosa."
Kabila aliingia madarakani akiwa na miaka 29 baada ya babake Laurent Desire Kabila kuuawa na mlinzi wake mwaka 2001.
Aliahidi kurejesha amani na kuangamiza ufisadi na amekuwa akitaja hayo kama baadhi ya mafanikio ya utawala wake.

DRC ilikuwa imekabiliwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe kati ya mwaka 1998 na mwaka 2003 ambapo takriban watu 5 milioni walifariki kutokana na vita, njaa na maradhi.
"Tuna majuto yoyote? La hasha, hata kidogo. Tumepata mafanikio mengi. Jambo kuu zaidi ni kwamba tuliweza…kuliunganisha tena taifa na kulirejesha kwenye mkondo ufaao."
Kabila amesema anataka kusalia katika siasa ili kulinda mafanikio hayo na kuongeza kwamba wanaotaka kutoa uamuzi kuhusu mafanikio yake wanaweza kusubiri hadi amalize kazi yake.
"Bado kuna safari ndefu sana mbele yetu na kuna sura nyingi sana ambazo zitaandikwa kabla tuanze kuandika vitabu vya historia."
Vital Kamerhe (kushoto) na Felix Tshisekedi
 Felix Tshisekedi ameungana na Vital Kamerhe ambaye ni mgombea mwenza wake

Katiba nchini DRC inamzuia mtu aliyeongoza kwa mihula miwili mfululizo kuwania tena urais, lakini haijazuia mtu kama huyo kuwania tena baada ya kiongozi mwingine kuingia madarakani.
Baadhi wanasema huenda kikawa kisa kama cha rais wa Urusi Vladimir Putin ambaye baada ya kuongoza kama rais kati ya 2000 na 2008, alikuwa waziri mkuu kati ya 2008 na 2012 kabla ya kurejea tena kama rais wa nchi hiyo. Alibadilishana na mwandani wake Dmitry Medvedev ambaye kwa sasa ndiye waziri mkuu.

Comments

Popular posts from this blog

Kiongozi wa Republican ahofia uongozi wa Trump

Kiongozi mmoja wa chama cha Republican nchini Marekani amesema kuwa anahofia maisha ya wajukuu wake saba ,chini ya uongozi wa rais mteule wa Marekani Donald Trump. Christine Todd Whitman ,ambaye ndio mkuu wa shirika la kulinda mazingira nchini Marekani amemshtumu Donad Trump kwa kupuuza ripoti za sayansi. Na amenonya kwamba tishio lake la kuondoa sera za kulinda hali ya anga linaweka siku za usoni hatarini. Wafuasi wa Trump wanasema kuwa sheria za hali ya anga na kawi zinaharabu biashara. Lakini Bi Todd Whitman amesema kuwa Marekani inapaswa kutafuta njia za kukuza biashara bila kuharibu mazingira. Maelezo kuhusu sera za mazingira za bw Trump hayajulikani ,lakini wanaomzunguka wanasema kuwa analenga kuimarisha mkaa, kufungua mabomba mapya ya mafuta, na kuruhusu uchimbaji madini msituni mbalii na kuchimba mafuta katika eneo la Arctic. Kisiasa ,wamependekeza kujiondoa katika makubaliano ya hali ya anga, kufutilia mbali sera ya rais Obama ya kupata kawi safi mbali na k...

Wasifu wa Jacqueline Ntuyabaliwe Mengi au K-Lynn

Haki miliki ya picha JACQUELINE NTUYABALIWE  Jacqueline Ntuyabaliwe (Jacqueline Ntuyabaliwe Mengi) ambaye pia anajulikana kama K-Lyn alizaliwa tarehe 6 mwezi Disemba 1978 mjini Dar es Salaam, Tanzania. Ni Mwanamuziki , mfanyabiashara na aliwahi kushinda taji la malkia wa Urembo nchini Tanzania (2000). Ni Mwanzilishi wa kampuni ya samani ilioshinda tuzo Amorette Ltd . Babake alitoka kutoka eneo la Kigoma akiwa daktari bingwa wa magonjwa ya wanawake huku mamake akiwa nesi. Alisomea elimu yake ya msingi katika shule ya bweni ya Nyakahoja Primary mjini Mwanza kabla ya kuelekea mjini Dar es Salaam ambapo aliendelea na elimu yake ya msingi katika shule ya Forodhani. Jackline ni msichana wa mwisho katika familia ya watoto watatu wa kike Katika utoto wake alikuwa msichana mwenye haya jingi lakini alipendelea sana kusoma vitabu Muziki Alianza usanii 1997 akishirikiana na bendi ya Tanzania kwa jina the Tanzanites. Aliimba kama mmojawapo wa viongozi kwa miaka mitatu. ...

Mwanza: Kibao kipya cha nyota Rayvanny na Diamond Platnumz chafungiwa na Basata

Kibao kipya kiitwacho, Mwanza, kilichotolewa na wasanii mashuhuri Tanzania Rayvanny na Diamond Platnumz kimepigwa marufuku na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata). Katika taarifa kwa umma iliyotolewa leo Novemba 12 Katibu Mtendaji wa Basata Godfrey Mngereza, sababu kuu ya kufungiwa wimbo huo ni ukiukwaji mkubwa wa maadili ya Kitanzania kwa "kutumia maneno yanayohamasisha ngono." Basata pia imeonya vyombo vya habari, na watu binafsi kutoutumia, kuucheza ama kuusambaza wimbo huo kwa namna yoyote ile. "Baraza linatoa onyo kali kwa msanii Rayvanny, Diamond Platnumz pamoja na uongozi wa Wasafi Limited kufuata sheria, kanuni na taratibu wakati wa kuandaa kazi za sanaa. Aidha Baraza limesikitishwa na kitendo hiki ambacho kimefanywa kwa makusudi," imeeleza taarifa hiyo iliyosainiwa na Mngereza. Wimbo huo wa Mwanza ulitolewa rasmi jana na tayari ulishavutia maelfu ya watazamaji kwenye mitandao ya kijamii. Wasanii hao wametakiwa kufuta kibao hiko katika kurasa...